Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mheshimiwa Daniel Chongolo, ametoa pongezi kwa Kaimu Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Ileje, Bw. David Gunza, kwa kazi nzuri ya ukusanyaji wa marejesho ya mikopo ya asilimia kumi inayotolewa na Halmashauri kwa vikundi vya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu kwa mwaka wa fedha 2021/2022 hadi 2023.
![]() |
Mheshimiwa Chongolo alitoa pongezi hizo wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani kilichoketi kujadili hoja za Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, ambapo alimtunuku Bw. Gunza zawadi ya shilingi laki tano (Tsh 500,000) kama ishara ya kuthamini juhudi na uwajibikaji wake.
Katika hotuba yake, Mkuu wa Mkoa aliwataka watumishi wengine wa umma kuiga mfano wa uadilifu na kujituma unaoonyeshwa na Bw. Gunza, akisisitiza kuwa mafanikio ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo yanategemea uwajibikaji wa kila mtumishi.
“Naomba niwasihi wote kuendelea kufanya kazi kwa bidii na uadilifu kwa maslahi ya wananchi na maendeleo ya taifa,” alisema Mheshimiwa Chongolo.
Mikopo hiyo ya asilimia kumi hutolewa kwa mujibu wa sheria kwa lengo la kuwawezesha kiuchumi makundi maalum katika jamii, na urejeshwaji wake unasaidia kuendeleza mfuko huo kwa wanufaika zaidi.
Haki Miliki Haki Zote Zimehifadhiwa