Mkuu wa Wilaya ya Ileje, Mheshimiwa Farida Mgomi, ametoa wito kwa wananchi wa Kijiji cha Msia, Kata ya Chitete, kuwa na utamaduni wa kutunza mazingira kwa kufanya usafi wa maeneo yao na kulinda vyanzo vya maji. Amesema utunzaji wa mazingira ni jukumu la kila mmoja na unapaswa kuzingatiwa kwa ajili ya ustawi wa jamii na kizazi kijacho.
Akizungumza wakati wa kilele cha maadhimisho ya Wiki ya Mazingira, DC Mgomi alieleza kuwa kaulimbiu ya mwaka huu isemayo “Mazingira Yetu na Tanzania Ijayo, Tuwajibike Sasa – Dhibiti Matumizi ya Plastiki” inapaswa kuchukuliwa kwa uzito mkubwa. Alisisitiza kuwa matumizi ya plastiki yasiyo na udhibiti yana madhara makubwa kwa mazingira na afya ya binadamu.
Aidha, aliwataka Maafisa Mazingira katika wilaya hiyo kuhakikisha wanakuwa na mipango kazi inayotekelezeka pamoja na mikakati ya kudumu ya kusimamia na kuzuia uharibifu wa mazingira. Alisema wasimamizi wa mazingira wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kutoa elimu, ufuatiliaji na kuhakikisha sheria za mazingira zinatekelezwa ipasavyo.
Maadhimisho hayo yalipambwa na burudani mbalimbali zikiwemo ngoma za asili, huku wananchi wakishiriki kwa wingi katika shughuli za usafi na utoaji wa elimu ya mazingira. DC Mgomi alitoa pongezi kwa wananchi waliojitokeza na kuahidi kuendelea kushirikiana nao katika kuimarisha uhifadhi wa mazingira wilayani Ileje.
Haki Miliki Haki Zote Zimehifadhiwa