Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika katika Wilaya ya Ileje yamefanyika kwa mafanikio makubwa katika kata ya Itale, yakihudhuriwa na viongozi wa serikali, wazazi, walimu, pamoja na wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali. Mgeni rasmi katika maadhimisho hayo alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Ileje, Mheshimiwa Farida Mgomi, ambaye aliwahimiza wazazi na walezi kuhakikisha wanawalinda na kuwa mstari wa mbele katika kutetea haki za watoto, ikiwa ni pamoja na kuwasaidia kutimiza ndoto zao kwa kuwa daraja la mafanikio yao ya baadaye.
Katika hotuba yake, Mheshimiwa Mgomi alitoa rai kwa jamii kuepuka na kukemea vikali vitendo vyote vya ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto, akisisitiza kuwa kila mtoto anapaswa kulelewa katika mazingira salama na yenye heshima. Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuwapatia watoto mahitaji ya msingi kama vile lishe bora, huduma za afya, elimu na malezi yenye upendo ili kuwawezesha kukua katika hali bora kimwili na kiakili
Sambamba na hayo, Mkuu huyo wa Wilaya alizitaka familia kuhakikisha zinawashirikisha watoto katika maamuzi yanayowahusu, huku zikihakikisha ulinzi na usalama wao unaimarishwa kila wakati. Alisisitiza kuwa ulinzi wa mtoto ni jukumu la kila mmoja katika jamii na akatoa wito kwa wadau wote kushirikiana katika kuhakikisha watoto wa Ileje na Tanzania kwa ujumla wanalelewa katika misingi ya haki, usawa na utu.
Haki Miliki Haki Zote Zimehifadhiwa