Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mheshimiwa Daniel Chongolo, ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Ileje kwa kupata hati safi kutoka kwa Mkaguzi wa Hesabu za Serikali.
Mheshimiwa Chongolo alitoa pongezi hizo leo tarehe 10 Juni 2025, wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika kwa ajili ya kujadili hoja za Mkaguzi.
![]() |
Kikao hicho kilihusisha wajumbe wa Baraza la Madiwani, wataalamu wa Halmashauri, pamoja na wajumbe wa Kamati ya Usalama kutoka ngazi ya Mkoa na Halmashauri.
Katika salamu zake, Mkuu wa Mkoa aliipongeza Halmashauri kwa usimamizi mzuri wa rasilimali za umma na uwajibikaji, akisema kuwa hatua hiyo ni kielelezo cha uwazi na uadilifu katika utendaji kazi wa Serikali za Mitaa.
“Kupata hati safi si jambo la kawaida – ni matokeo ya juhudi, uadilifu na uwajibikaji wa pamoja. Nawaomba muendelee kushikilia viwango hivi vya uwajibikaji kwa maslahi ya wananchi wetu,” alisema Mheshimiwa Chongolo.
Aidha, aliwataka viongozi na watendaji wa Halmashauri ya Ileje kuendelea kushikilia viwango vya juu vya utendaji kazi na kuhakikisha kuwa mapendekezo yote yaliyotolewa na Mkaguzi yanatekelezwa kwa wakati.
Kwa upande wao, madiwani na viongozi wa Halmashauri walimshukuru Mkuu wa Mkoa kwa uongozi wake na usimamizi makini, na kuahidi kuendelea kushirikiana kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa Ileje.
Haki Miliki Haki Zote Zimehifadhiwa