Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ileje, Bi Nuru Waziri Kindamba, ameongoza hafla ya kuwaaga madaktari bingwa wa Mama Samia waliokuwa katika kambi maalum ya matibabu ya kibingwa katika Hospitali ya Wilaya ya Ileje. Hafla hiyo ilifanyika kwa ajili ya kuwashukuru madaktari hao kwa mchango wao mkubwa katika kutoa huduma bora kwa wananchi wa Ileje. Bi Kindamba alieleza kuwa kambi hiyo imeleta unafuu mkubwa kwa wananchi waliokuwa wakihitaji huduma za kibingwa. Pia alitumia fursa hiyo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuboresha sekta ya afya nchini.
Aidha, Bi Kindamba aliwataka madaktari bingwa kuendelea kushirikiana na wenzao wa Hospital ya Wilaya ya Ileje ili kuimarisha utoaji wa huduma za afya kwa kubadilishana uzoefu. Alieleza kuwa ushirikiano huo utasaidia kuboresha ujuzi wa wataalamu wa afya na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma. Pia alisisitiza umuhimu wa kuwa na mawasiliano ya kudumu kati ya madaktari bingwa na wale wa wilaya. Ushirikiano huo utakuwa chachu ya maendeleo ya huduma bora kwa wananchi.
Katika hatua nyingine, Bi Kindamba aliwasihi Madaktari wa hapa Ileje kutumia vyema elimu na uzoefu walioupata kutoka kwa madaktari Bingwa. Alisema uzoefu huo ni hazina kubwa itakayowasaidia katika kutoa huduma bora na zenye ufanisi zaidi. Aliongeza kuwa serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa watumishi wa afya. Hafla hiyo ilihitimishwa kwa shukrani na pongezi kwa madaktari Bingwa kwa mchango wao mkubwa kwa jamii ya Ileje.
Haki Miliki Haki Zote Zimehifadhiwa